1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaMarekani

Mkutano wa Demokrasia chini ya Marekani kuanza Jumanne

27 Machi 2023

Mkutano wa pili wa kilele wa Demokrasia utaanza rasmi hiyo kesho nchini Marekani ambayo inatafuta uungwaji mkono dhidi ya utawala wa kiimla.

https://p.dw.com/p/4PIE8
Kanada US-Präsident Joe Biden spricht vor dem kanadischen Parlament in Ottawa
Picha: Blair Gable/REUTERS

Mkutano huo umeitishwa wakati Urusi ikiishambulia Ukraine na China ikijizatiti kidiplomasia.

Rais Joe Biden alichukua madaraka akiahidi kutetea demokrasia, na katika mwaka wake wa kwanza alitekeleza ahadi hiyo kwa kuandaa mkutano kama huo ambapo alitaka kuthibitisha tena uongozi wa Marekani baada ya mtangulizi wake Donald Trump kufuta kanuni za kidemokrasia kufuatia mashambulizi ya Bunge.

Kwa jumla Biden amewaalika viongozi 121 katika mkutano huo wa siku tatu utakaofanyika kwa njia ya kimtandao.

Vikao hivyo vitawaleta pamoja wawakilishi wa mashirika ya kiraia kwa ajili ya majadiliano juu ya changamoto mbalimbali za demokrasia ikiwa ni pamoja na teknolojia ya ulinzi, ambayo Marekani inaona kuwa tishio linaloongezeka kutokana na China kufanya maendeleo ya haraka ya teknolojia.